THE OVERSIGHT ROLE OF TANZANIA MINERAL AUDIT AGENCY (TMAA)
LAANA YA RASILIMALI KATIKA SEKTA YA MAFUTA NA GESI ASILIA- Je Tanzania Inaweza Kuepuka Laana Hiyo Kihalisia
1. LAANA YA RASILIMALI KATIKA SEKTA YA MAFUTA NA GESI ASILIA- Je
Tanzania Inaweza Kuepuka Laana Hiyo Kihalisia?
Na: Prof Handley Mpoki Mafwenga Simba
Ph.D (Finance), MSc (Finance), MBA (Mg.Eco), LLM (Taxation), PGDTM, LLB, ADTM, ICSA (UK)
[Mchambuzi wa Sera za Uchumi, Bajeti na Kodi]
Laana ya rasilimali au Kitendawili cha Utajiri wa rasilimali ni pale ambapo Tanzania
ina uwingi wa maliasili, hasa mali ghafi yenye thamani kubwa kama vile mafuta na
gesi ambayo huendana na ukuaji mdogo wa Uchumi na matokeo mabovu ya
Maendeleo kama vile kuongezeka kwa Umaskini, kutokuwepo kwa hali ya Usawa
katika jamii na huduma dhaifu za Umma. Nchi inayotegemea sana kuuza mafuta
na gesi nje ya nchi, huzalisha mapato makubwa yanayopelekea bila kufahamu
uwepo wa Uchumi uliodumaa na hali ya kisiasa isiyo imara. Nchi zenye maliasili
nyingi za mafuta na gersi na ukuaji mdogo wa Uchumi ni Gabon, na Nigeria
ambazo zilikuwa kati ya nchi Hamsini tajiri Duniani kwenye miaka ya sabini na kwa
sasa zimetokea kuwa ndiyo nchi Maskini za kwanza Duniani zinazozalisha mafuta
na gesi ikiwemo Nchi ya Zambia. Aidha, zaidi ya nusu ya Wananchi wa Msumbiji
nchi ambayo pia ina utajiri wa mafuta na gesi wanaishi ndani ya wimbi la
Umaskini pamoja na maliasili nyingi walizonazo. Hii inaonesha kuwa mafuta na
gesi hunufaisha Kampuni za kigeni za Kimataifa na Wanasiasa.
Swali la kujiuliza ni kuwa; Kwanini Nchi kama Tanzania inapaswa kutegemea
mafuta, gesi na madini katika Uchumi wake? Ukweli ni kuwa wakati chanzo chake
kikubwa cha mapato ni uuzaji wa malighafi Kwenye Soko la Kimataifa, Uwekezaji
kutoka nje na Teknolojia vinahitajika kutumika katika maliasili hizo na Uwekezaji
hufanywa na Kampuni za Kimataifa zenye Uwezo mkubwa. Tarakibu ya Ugonjwa
wa Kidachi unalenga Kwenye uhamaji wa mahitaji kutoka kwa Wawekezaji. Nchi
kama Gabon inazalisha Zaidi ya mapipa 300,000 ya mafuta kwa siku. Ni nchi
inayopata mvua za kitropiki lakini ni vigumu kupata hata zao la ndizi ambalo
huzalishwa sana Nchini Cameroon. Gabon ni nchi ambayo ina sekta ya kilimo
yenye nguvu, lakini kitendo cha kutegemea mafuta kuuza nje ya nchi
kumedhoofisha matumaini ya Maendeleo endelevu. Nchi ya Zambia katika hali ya
kawaida, kiwango cha kubadilisha fedha za kigeni kilipanda kwa asilimia 15%
2. katika robo ya kwanza ya Mwaka, 2008 ukilinganisha na hali ya robo ya kwanza ya
Mwaka, 2005 kwa ajili ya kukua kwa zao la Mafuta. Ukuaji wa bei ulisababishwa
na kupanda kwa thamani ya fedha yao ya Kwacha ambayo pamoja na kuwepo
kwa Biashara huria kulisababisha kilimo cha uzalishaji kupungua. Zambia haina
udhibiti wa Mitaji, ilipunguza Ushuru wa forodha na ilijiingiza katika Utaratibu wa
kubadilisha fedha za kigeni kwa kuzingatia soko la fedha na hali ya Uchumi uliopo.
Picha Na 1: Utaratibu na Muundo wa Laana ya Rasilimali
Tarakibu ya Uchumi Jumuishi wa Kisiasa inachambua Motisha na Vikwazo vya
Serikali. Mifumo yake ina dhana isemayo “Kodi ni chanzo cha Laana ya rasilimali” .
Kodi kwenye rasilimali kunasababisha ukosefu wa tija na ukengeufu wa tabia
katika nchi yenye Taasisi dhaifu, isiyoweza kutafuta vyanzo vingine vya mapato na
kuwa na Usimamizi imara wa Mapato. Nadharia ya Uhai wa Mzunguko wa Kodi ni
kitu kikubwa kukiangalia katika Sekta ya Mafuta na Gesi. Nadharia hii inahitaji
Kodi iwe kwenye mzunguko kupitia kwenye masoko kuliko kuwekwa na Serikali.
Katika nchi zenye Kodi kubwa maliasili huhamasisha dhana ya Kisiasa kuwa na
miliki, wakati ambapo nchi zenye Kodi ndogo Serikali lazima iwape motisha watu
wake kuwa na utajiri. Hii husababisha kupata manufaa ya Uoanishaji wa kiuchumu
na Kukuza Usawa ndani ya Jamii ikiwa ni pamoja na Kukuza Taasisi za Kiraia kwa
ujumla. Mfano; Nchi ya Gabon imekuwa ikishuhudia kushuka kwa hifadhi ya Kodi
kubwa iliyokuwa imewekwa.
3. Mazingira magumu yaani Vulnerability ni aina ya Laana ya Rasilimali ambayo
inasababishwa na myumbo mkubwa wa bei za bidhaa za mafuta. Nchi zenye
utajiri wa maliasili mara nyingi zinakabiliwa na Matumizi makubwa ya fedha
zitokanazo na Mafuta yaani “Mzunguko wa Ukuaji na Mpasuko wa Mapato”. Hii
ni kwasababu, Maliasili zinahama kwa kuzingatia shinikizo la Mahitaji; hata hivyo,
kama kutakuwa na Uchumi ambao una Muundo wa kuuza mafuta nje
kutasababisha na Mazingira magumu kutokana na myumbo wa bei kwenye
mafuta na gesi. Kukua kwa Sekta ya mafuta na gesi kulikosababishwa na kupanda
kwa bei ya maliasili hizo katika soko la Dunia au kwa kuwa na kupata mafuta
mapya kwenye uchimbaji kunasababisha ukuaji wa mapato kwa nchi, ambapo pia
husababisha kuongezeka kwa Uingizaji wa bidhaa kutoka nje na Matumizi ya
ndani kwa bidhaa zote za Kibiashara na zisizo za Kibiashara.
Katika Laana ya rasilimali, Utajiri wa maliasili ya mafuta na gesi unahamasisha nchi
kujiingiza kwenye Mikopo iliyokithiri ambapo maliasili hizo huwa ni dhamana ya
Mkopo. Aidha, Hali ya kutokuwa na uhakika wa mapato ya maliasili hizo
husababisha Usimamizi mbovu wa Mapato kwa kufanya matumizi ya mapato
hayo hata pale ambapo kuna miradi isiyo ya kudumu; na hii hutokea wakati wa
ufinyu wa Bajeti au kama kuna ukosefu wa Uwezo wa kufanya matumizi au kuna
Mzunguko wa Ukuaji na Mpasuko wa Mapato ambapo Matumizi hupanda na
kushuka bila mpangilio wowote wa maana. Kwavile Mafuta na Gesi na uzalishaji
wake una myumbo mkubwa katika Uchumi, Serikali nyingi zinazotegemea
rasilimali hizo husababisha Mzunguko wa Sera ya Bajeti kuwa na tabia ya
kuongeza Matumizi wakati Mapato ya Mafuta na Gesi yako juu na pia Sera hiyo
huwa na tabia ya Kupunguza Matumizi wakati Mapato yameshuka.
Athari za Ukuaji wa rasilimali katika Uchumi ni Jambo kubwa la kufanyiwa
tathmini. Ukuaji wa maliasili unaathiri Uchumi katika njia mbili (1) Athari za
Uhamaji wa maliasili ambapo uongezekaji wa bei kwenye Sekta ya Nishati
unaongeza thamani ya ongezeko la uzalishaji wa ajira katika Sekta ya Nishati na
unaondoa Msawazo wa malipo ya ajira kwa kuongeza malipo ya ajira kuwa juu, hii
inasababisha ajira kuhama kutoka kwenye Sekta za uzalishaji na Sekta zisizo za
kibiashara kwenda kwenye Sekta ya Mafuta na gesi. Hii ni kwavile watu hupenda
kulipwa Mishahara mikubwa muda wote.
Uhamaji wa Soko la ajira hutokea kwavile Sekta mbalimbali katika Uchumi
hushindana kwa kuajiri Wafanyakazi wenye Ujuzi na kwavile kuna uhaba wa Ujuzi
katika soko la ajira ndipo huwa rahisi Waajiriwa kuhamia kwenye Sekta ya Nishati
na Mafuta ambako kuna Mshahara mkubwa. Athari zake kubwa ni bei za ndani
4. kuwa juu na hii husababisha kupungua kwa Ushindani kwenye bidhaa zitokanazo
na Sekta za Kibiashara za kuuza bidhaa nje na kununua bidhaa mbadala kuzileta
nchini.
Picha Na 2: Myumbo wa Sera Za Bajeti Kati ya Ukuaji wa Mapato na Matumizi ya Serikali
Tanzania inaweza isiepuke na laana ya rasilimali kwa sababu ya Myumbo wa
Uchumi hasa Ugumu wa kukadiria Kiwango cha Mapato. Kuna ugumu wa
kukadiria na kupanga Kiwango cha Mapato, Kupanga Bajeti na Kufanya Matumizi
kwa sababu ya Myumbo wa mapato ya rasilimali unaosababishwa na bei za
bidhaa na Ukosefu wa Ujuzi maalum na Elimu ya Tasnia ya Uziduaji ambayo
inaweza isiwe ya kutosha Tanzania. Mfano, Nigeria Mnamo Mwaka, 2006
ilikadiriwa kupata kiasi cha Dola za Marekani Bilioni 36 kila Mwaka kutoka kwenye
Tasnia ya Petroli; makadirio mengine ni kiwango cha Mapato yanayokadiriwa
kuwa Zaidi ya Bilioni 45. Hata hivyo, ndani ya Miaka Hamsini ya ongezeko la
uzalishaji wa mafuta na gesi, Nigeria imebaki kuwa ni nchi maskini kati ya nchi
maskini Duniani zenye Miundombinu ya Jamii mibovu.
Je Tanzania Inaweza Kuondokana na Laana ya Rasilimali?
Tanzania inaweza kuepukana na Laana ya rasilimali kwa Kuzingatia Mambo
yafuatayo;
5. kupunguza Rushwa na Utawala Mbovu; Nigeria kwa Mfano hali ya rushwa na
utawala mbovu bado uko juu na ni nchi ambayo inakadiriwa kupoteza dola bilioni
380 kwa ajili ya rushwa na huu ni upotevu kati ya Mwaka 1960 hadi 1999. Tangia
hapo, hali imekuwa mbaya Zaidi hata kwenye Sheria za Uraia, pamoja na juhudi
kubwa zilizofanywa na Asasi ya kupambana na rushwa iitwayo Economic and
Financial Crime Commission (EFCC), ikiwemo pia Asasi ya Independent Corrupt
Pratices Commission (ICPC) na Taasisi ya Kimataifa ya Uwazi iitwayo Transparency
International iliyo chini ya Benki ya Dunia. Nchi ya Guinea imeingia katika
Mikataba mingi kwa njia ya rushwa ambayo imesababisha kuwepo na Mikataba
mibovu. Katika Mwaka, 2012 nchi ya Guinea ilifanya marejeo ya Mikataba ya
Utafiti wa Madini ya Chuma na yatoayo zao la Alumini (Bauxite). Katika Mwaka,
2011 Guinea ilitunga Sheria mpya ya madini inayokidhi Viwango vya Kimataifa na
Kukuza Uwazi na Utawala Bora.
Ili Tanzania ifanikiwe kuondokana na laana ya rasilimali, inabidi iongeze jitihada ya
kupambana na rushwa. Izibe mianya ya ushawishi wa rushwa kutumia Sheria na
Kanuni ikiwa ni pamoja na kuboresha Utawala wa Sheria; kuboresha Usimamizi
wa Haki za Binadamu; Kuimarisha Taratibu za Kidemokrasia na Asasi zake;
kuongeza Usimamizi wa ngazi zote za Serikali; Huduma za raia ikiwa ni pamoja na
Polisi na Jeshi; na Mahakama; Kufafanua vizuri Zaidi Haki za Umiliki wa Mali katika
maeneo yote ya rasilimali za kwenye maeneo ya Uchimbaji yaliyopo kwa Wazawa.
Ili kupata Maana ya rushwa na kuziba mianya kwenye Sheria na Kanuni ni vyema
kurejea Kanuni ya Hesabu ifuatayo;
Rushwa=[Mamlaka+ Uwezo wa Hiari+Wajibu]-Uwajibikaji
Kupitia kwenye Uchumi na Mipango Mseto; Tanzania yafaa ihusike na Uchumi
mchanganyiko kwa kuachana na kuhangaika na Sekta za Mafuta pekee na
Kufungamanisha Sekta hiyo na Sekta zingine kama Uwekezaji kwenye Kilimo na
Kuboresha Uzalishaji. Kujenga Viwanda ikiwa ni pamoja na Huduma kama vile
Teknolojia ya Habari, Usafirishaji na Huduma za kutoka nje ya Nchi zinazopitia
Tanzania ili kuzinusuru kuwa katika mrundikano wa Uchumi na Sekta ya Mafuta.
Kuboresha Myororo wa Usambazaji wa Bidhaa na Huduma ndani ya Sekta ya
rasilimali; iwe kupitia kwenye eneo la Bahari Kuu kufungamanisha na Tasnia
zingine za rasilimali, au kupitia kwenye Uimarishaji wa Ufungamanishaji na
rasilimali msingi na Viwanda vya Uchakataji nje ya Bahari Kuu. Mfano, Wazalishaji
wa Mafuta kama nchi ya Angola na ya Chad hazina Uchumi Mseto na ni moja ya
Nchi Maskini kutokana na Uwiano wa Kipato wa asilimia 64% na Idadi kubwa ya
watu iko chini ya Mstari unaopima kiwango cha Umaskini. Lakini, Nchi nyingine
6. zinazozalisha mafuta zilizofanikiwa katika Kuwa na Uchumi Mseto ziko katika
kiwango kizuri katika kipimo cha Umaskini; nchi hizo ni kama Indonesia na
Malaysia. Nchi ya Nauru imefaidika sana na kiwango cha juu cha Ukuaji Uchumi
baada ya kupata Uhuru kutokana na uchimbaji mkubwa wa madini ya phosphate.
Kwa matarajio ya kumalizika kwa uchimbaji wa madini hayo, uwekezaji mkubwa
ulifanywa kwenye Mifuko ya Dhamana kusaidia kusukuma hali ya Mpito na
kufanya Uchumi wa baadaye wa Nauru uwe imara. Hata hivyo, kwa sababu ya
Matumizi makubwa kutoka kwenye Mifuko ya Dhamana, ikiwa ni pamoja na
shughuli za uwekezaji zisizo na tija, Serikali iliishia kuwa na hali ya Kufirisika.
kuchanganya Sera imara za Bajeti na za Uchumi Jumla ili kuzuia laana ya
rasilimali; Iwapo Tanzania itachanganya Sera husaidia kuzuia Uchumi wa ndani
kwenye Myumbo wa Mapato ya bidhaa na hivyo husaidia kuwa na Bajeti Imara na
Endelevu. Mfano, Nchi ya Botswana ilipitisha Sera imara ya Uchumi Jumla dhidi ya
Ugonjwa wa Kidachi. Ikiwa na Usimamizi mzuri wa Matumizi, Botswana iliweza
kuondokana na Matumizi mabaya wakati wa kipidi chake cha neema ya Mapato
na ilijizuia katika Kukopa kipindi ambacho Mapato yalishuka. Hii iliwezesha
Botswana iweze kupandisha kiwango cha ukuaji Uchumi kutoka Nchi ya 25 kati ya
nchi Maskini Mwaka 1966 hadi kufikia nchi ya Juu yenye Kipato cha Kati ndani ya
Miaka 30. Myumbo wa Uchumi una athari katika ukuaji wa Uchumi. Kiwango cha
kubadilisha fedha za kigeni hupanda wakati wa Mzunguko wa Neema ya Mapato
na wakati wa bei kuwa juu kwenye soko la Kimataifa la bidhaa, na hupungua
wakati wa Mzunguko wa Mpasuko wa Mapato kwa ajili ya Matumizi. Hii huathiri
nidhamu ya Kibajeti, udhibiti wa fedha za Umma na Mipango ya muda mrefu.
kupitisha Nadharia ya Urithi wa rasilimali kwa kizazi kijacho na Ugawanyaji wa
Maliasili; Hii ina maana Tanzania inapaswa kuwekeza katika Kilichowekezwa, na
kuanzisha Mfuko wa Mapato nje ya Nchi yaani “Sovereign Wealth Fund”. Kuunda
Mifuko ya mafuta na gesi ambayo ni ya aina mbili; (1) Mfuko wa Kuimarisha
Mapato ambao unapunguza athari za myunbo wa bei za rasilimali katika Uchumi
na unaboresha Uhakika wa Bajeti kwa Kuimarisha aina ya Matumizi; (2) Mfuko wa
Kuhifadhi Mapato ambao unahakikisha kuwa Uwiano wa Utajiri wa rasilimali
utakuwepo muda wote kwa ajili ya Kizazi kijacho hata baada ya rasilimali
zitakapokwisha. Mfano, Mfuko wa kudumu wa Alaska yaani Alaska Permanent
Fund unahifadhi Mapato ya Sekta ya Mafuta na unagawa nusu ya mapato
yaliyowekezwa kwa uwiano sawa, raia wanajua kwa kiwango gani watumie fedha
zao kwa ubora Zaidi kuliko hata Serikali inavyoweza kufanya; Mifuko mingine ni
kama ule Mfuko wa Nchi ya Norway uitwao State Petroleum Fund, Mfuko wa Nchi
ya Venezuela uitwao Venezuela Stabilization Fund na Mfuko wa Nchi ya Kuwait
7. uitwao Kuwait Reserve Fund. Nchi ya Botswana pia ina Mfuko uitwao Pula Fund
ambao unahifadhi Mapato kutoka kwenye madini ya Almasi. Mfuko huu
umewekezwa kwenye dhamana zilizothamika katika fedha za kigeni kama Mfuko
wa Hifadhi ili kukabili ushukaji wa thamani wa Almasi na kama lindo la kifedha
dhidi ya Myumbo wa Uchumi.
Picha Na 3: Muundo wa Mambo Muhimu ya Mfuko wa Kuhifadhi Mapato ya Mafuta na Gesi
Kutegemea na Malengo ya Sera Ambayo Malengo ya Mfuko Yatafikiwa
LENGO MUHIMU LA
SERA
MAELEZO
Uimarishaji Kuhakikisha Uzuiaji wa Myumbo wa Sera ya Bajeti ambayo inaweza kuzuia athari za
myumbo mkubwa wa bei za bidhaa kwenye Mapato ya Mafuta
Tahadhari Kulinda dhidi ya mabadiliko yasiyo ya kawaida katika hali ya Matumizi ya nchi kwenye
Bajeti (Mfano: Maafa ya asili, Vita n.k)
Hifadhi kwa ajili ya
Kizazi Kijacho
Kuweka Mapato kwa ajili ya Kizazi kijacho au mahitaji ya kizazi kilichopo
(Mfano: Mahitaji ya Mafao ya Uzeeni ya baadaye yaani Pensioni)
Kuhakikisha Kizazi Kijacho kinafaidi rasilimali zetu sawa na Kizazi
kilichopo
Uwekezaji Kuweka Matumizi endelevu ya muda mrefu (kubuni vynazo vipya vya
mapato nje ya rasilimali za mafuta na gesi)
Kusaidia Wananchi au Maendeleo ya Uchumi ya Taifa
Kwa Kukosekana kwa fursa zilizopo kwa ajili ya Uwekezaji wa ndani au
Matumizi ambayo hutoa manufaa sawa na yaliyopo kama vile Uwekezaji
wa Kifedha.
Dhana ya Ushirikishwaji wa Umma, Uwekezaji wa ndani wa Sekta binasfi, Uwazi
na Uwajibikaji; Uwazi na Uwajibikaji unapatikana kama Tanzania itashirikisha
Umma katika Usimamizi wa Mapato kwa ajili ya kudhibiti utegemezi kutoka nje ya
nchi. Taasisi kama Asasi zisizo za Serikali za Kimataifa, Benki ya Dunia, na Asasi ya
Uwazi katika Tasnia ya Uziduaji yaani (EITI) ndizo zenye kuhusiana nazo sana.
Asasi ya Uwazi katika Tasnia ya Uziduaji inashauri kufuata Viwango vya Kimataifa
vya Uadilifu kuhusiana na Viwango vya ajira, kuepuka vitendo vya rushwa na
kulipa kodi stahiki kwa Serikali inayotokana na rasilimali zetu.
Uimarishaji wa Wajibu kwa Jamii (CSR) na Uwezeshaji na Ushirikishwaji wa
Wananchi; Wajibu wa Kampuni za Kimataifa ni kuhakikisha zinawajibika kwa
jamii. Mfano, Nchi ya Angola ina historia ndefu katika Sekta ya Mafuta na Gesi
Zaidi ya miaka 30 sasa ukilinganisha na nchi nyingine za Afrika. Hata hivyo, ajira za
ndani na Uwezeshaji na Ushirikishwaji wa Wananchi bado upo chini sana. Nchi
kama Norway toka ilipoanza kuchimba mafuta mika ya 1960, imeishia kwenye
kiwango kidogo cha Uwezeshaji na Ushirikishwaji wa Wananchi kwa kuwa na
Wageni tu kwenye maeneo ya Bahari kuu na nje ya Bahari Kuu ikiwa ni pamoja na
8. Myororo wa Usambazaji bidhaa na huduma uliopo. Ajabu ni kuwa kwa Miuongo
mitatu iliyopita Uwezeshaji na Ushirikishwaji kwa Norway ilikuwa asilimia 70% na
sasa umeshuka hadi asilimia 50%.
kuimarisha Uwezo na kuepukana na Ufanisi mbovu wa Serikali; Tanzania
inakabiriwa na Changamoto hizi za Kusimamia utajiri wa rasilimali kwa dhana ya
kuendeleza shughuli za Uchumi. Uwezo na Ufanisi wa Serikali unaweza kuathiriwa
na Miundo mibovu ya nchi ikiwa ni pamoja na Mifumo ya Usimamizi, Matumizi
mabovu ya Mapato kwa muda mfupi, na Kukosekana kwa Uwezo. Mifumo mibovu
kama vile Utawala wa Sheria na Udhibiti wa rushwa unaruhusu Matumizi mabaya
ya Mapato na hivyo kuishia kuwa na Serikali ya Ukandamizaji. Mfano, Nchi ya
Equatorial Guinea kutokana na Mifumo mibovu ya Serikali na Uhaba wa Programu
za Jamii unaifanya Serikali kupata shida kuhudumia Wananchi wake.
Katika nchi ya Msumbiji, rushwa na matatizo ya Wanasiasa katika shughuli za
Biashara na zabuni za Serikali ni tatizo kubwa. Mnamo Mwaka, 2011 Kipimo cha
Mitizamo ya Uwazi na Rushwa yaani “Transparency International Corruption
Perceptions Index” kiliiweka Msumbiji kuwa na kiwango cha Uwiano wa 2.7 kwa
kipimo cha kuanzia sifuri hadi namba kumi wakati sifuri ina maanisha nchi yenye
kiwango kikubwa cha rushwa na kumi ina maana ya nchi kuwa safi bila rushwa.
Msumbiji ina Uwezo mdogo na itakuwa muhimu kwa Serikali kujenga Uwezo
katika kuzuia rushwa, na kuweka jukwaa la Mazungumzo kati ya Serikali na raia na
kati ya Serikali na Vyama vya Upinzani.
Kuweka Mfumo Imara wa Kanuni za Bajeti; Kanuni za Bajeti ni za miaka
mbalimbali yenye dhana ya kuhusika na Vikwazo dhidi ya fedha za Serikali
ambapo hubainishwa kwa malengo yanayowekwa kwa nambari. Tanzania
inapaswa kuwa na Kanuni za Bajeti ambayo ni hatua ya kuweka dhamira,
inayolazimisha Serikali kuwa na malengo ya muda mrefu ya Bajeti na hivyo, huwa
ni Dira ya muda mrefu kwa ajili ya Usimamizi wa Fedha za Umma. Kanuni hizi
zinazuia Matumizi mabaya na huzuia Serikali kuzidisha Matumizi haraka. Kanuni
hizi huihamasisha Serikali kuweka Sera ya Bajeti ya Kuzuia Myumbo wa Fedha na
huzuia athari mbaya zitokanazo na Myumbo wa Mapato. Aidha, zinakuza
Uaminifu kwa Serikali dhidi ya dhamira yake ya kuweka Sera za Bajeti Imara
zinazoweza kuchochea Uwekezaji kwa Sekta binafsi. Kwa Mfano, nchi kama Chile
ina Kanuni za Bajeti ambazo zinaweza kutoa mfano mzuri wa Sera imara ya Bajeti.
Nchini Chile Muundo wa Kanuni Sawia wa Bajeti hufanya Serikali ione rahisi
kutekeleza Sera za kupambana na Myumbo wa Uchumi kwa kuwa na uwezo wa
kukabili ufinyu wa Bajeti wakati wa hali mbaya ya Uchumi na kujenga Uchumi
9. bora wakati wa hali nzuri ya Uchumi. Kanuni inayojumuisha hisa au hifadhi na
mtiririko wa mambo mengine imeundwa kwa kulenga Kiwango cha Muundo wa
Bajeti yenye ziada yaani ‘structural’ fiscal surplus rate (SFSR) kwa asilimia 1% ya
mwenendo wa kiwango cha ukuaji Uchumi.
Kuimarisha Ukadiriaji wa Mapato ya rasilimali za Taifa; Huu ni Mfumo wa Sera
ya Uchumi Jumla na wa Bajeti. Tanzania inapaswa Kuimarisha uwezo wa kubuni
na kuhakiki mifumo ya Bajeti ya muda wa kati na ya muda mrefu na hata kuunda
Bajeti za Mwaka. Hii inapaswa kwenda pamoja na kupitisha Tarakibu ya Kukuza
maeneo ya kiuchumi kwenye kila miradi ya rasilimali. Kuwa na Mazingira imara ya
Uwekezaji na yenye kutabirika kwenye Sekta ya gesi kukua; ambayo itahusisha
kuheshimu Mikataba na Haki za Kumiliki mali kama vile Mikataba ya Uzalishaji na
Ugawanaji Faida; Kuwapa Wawekezaji Mazingira ya Kujiamini kuwa watabaki
katika milki ya miradi yao.
MUNGU IBARIKI TANZANIA, MUNGU IBARIKI AFRIKA”