1. Kwa jina la Allah Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu
Hamdu zote ni zake Mwenyezi Mungu Mola wa walimwengu na sala na salamu zimshukie
Bwana wa Manabii na Mitume wa Mwenyezi Mungu na Aali zake watukufu na masahaba zake
wema.
Kuwadia kwa msimu wa Hija kunapaswa kutambuliwa kuwa ni sikukuu kubwa ya Umma wa
Kiislamu. Fursa kubwa inayoletwa na siku hizi zenye thamani katika miaka yote kwa Waislamu
duniani ni kemia inayofanya muujiza ambayo iwapo itathaminiwa ipasavyo na kutumiwa vizuri
inaweza kutibu magonjwa mengi ya ulimwengu wa Kiislamu.
Hija ni chemchemi ya baraka tele za Mwenyezi Mungu. Ninyi Mahujaji mliopata saada,
mumepata fursa ya kuosha nyoyo zenu katika amali na ibada hii iliyojaa usafi na umaanawi na
kutumia hazina hii ya rehma, izza na qudra kwa ajili ya kujiwekea akiba ya umri wenu wote.
Msimu huu wa ibada ya Hija ni shule ya kujifunza na kujistawisha ambayo ina masomo ya kuwa
wanyenyekevu na kujisalimisha kwa Mola Mlezi, kubeba majukumu waliyopewa Waislamu na
Mwenyezi Mungu, kufanya jitihada, nishati na harakati katika kazi za dini na dunia,
kurehemeana na kusameheana katika kuamiliana na ndugu, masomo ya ushujaa na kujiamini
katika kukabiliana na matukio mazito na kuwa na matumaini na msaada wa Mola Karima katika
kila mahala na katika kila kitu. Kwa ufupi tunasema kuwa, msimu wa ibada ya Hija ni uwanja
wa kujenga shakhsia ya mwanadamu kwa mujibu wa vigezo vya Kiislamu. Kwa msingi huo
mnaweza kujipamba humo kwa vito hivyo vya kiroho na kufaidika na hazina hiyo tukufu na
kuchukua matunda yake kwa ajili ya nafsi zenu na zawadi kwa nchi, mataifa yenu na Umma
mzima wa Kiislamu.
Hii leo Umma wa Kiislamu unahitajia zaidi wanadamu wanaoambatanisha pamoja amali, imani,
usafi wa roho, ikhlasi, muqawama mbele ya maadui wenye vinyongo pamoja na kuijenga nafsi
kiroho na kimaanawi. Hii ndiyo njia pekee ya wokovu wa jamii kubwa ya Waislamu kwa kipindi
kirefu kutoka kwenye matatizo iliyotumbukia ndani yake ama kwa mikono ya adui au kutokana
na udhaifu wa azma, imani na busuri.
Hapana shaka kuwa kipindi cha sasa ni kipindi cha mwamko na kupata utambulisho wa
Waislamu; uhakika huu unaweza kuonekana waziwazi kupitia changamoto zinazozikabili nchi za
Waislamu. Ni katika mazingira haya ndipo azma na irada inayoegamia kwenye imani,
kutawakali kwa Mwenyezi Mungu, kuona mbali na tadbiri vinapoweza kuyapatia ushindi na
fahari mataifa ya Waislamu katika changamoto hizi na kuyafikisha kwenye mustakbali wenye
izza na utukufu. Kambi nyingine ambayo haiwezi kustahamili mwamko na izza ya Waislamu,
imejitosa katika medani kwa nguvu zake zote na inatumia nyenzo zake zote za kiusalama,
kinafsi, kijeshi, kiuchumi na kipropaganda kwa ajili ya kuwatibua na kuwakandamiza Waislamu
na kuwashughulisha wao kwa wao. Hali ya nchi za magharibi mwa Asia kuanzia Pakistan hadi
Syria, Iraq na Palestina, nchi za Ghuba ya Uajemi, na vilevile nchi za kaskazini mwa Afrika
kuanzia Libya, Misri na Tunisia hadi Sudan na baadhi ya nchi nyingine, inaweka wazi mambo
mengi. Vita vya ndani, taasubiri kipofu za kidini na kimadhehebu, machafuko ya kisiasa, kuenea
ugaidi uliojaa ukatili, kujitokeza makundi na mirengo yenye misimamo ya kufurutu mipaka
ambayo yanatumia mbinu za kaumu zilizokuwa zikiishi maisha ya kishenzi katika historia kama
kupasua vifua vya wanadamu na kutafuna nyoyo zao, watu wanaobeba silaha wanaoua watoto na
wanawake, watu wanaochinja vichwa vya wanaume na kuwabaka wanawake na wakati
mwingine kufanya jinai hizo za kukirihisha na kuchafua moyo kwa kutumia jina na bendera ya
dini, yote hayo ni matokeo ya mpango wa kishetani na kibeberu wa mashirika ya kijasusi ya
wageni na tawala vibaraka wao katika Mashariki ya Kati na kaskazini mwa Afrika ambayo
yanatayarisha mazingira ya ndani kwa ajili ya matukio hayo na kuyaonjesha shubiri mataifa
2. mbalimbali. Ni wazi kuwa katika hali kama hii hatuwezi kutarajia kuwa nchi za Waislamu
zitajaza mapengo yao ya masuala ya kimaanawi na kiroho na kupata amani, hali bora ya maisha
na maendeleo ya kisayansi na nguvu ya kimataifa ambavyo ndiyo baraka za mwamko na kupata
utambulisho wa Kiislamu. Hali hii ya maafa inaweza kuutia ugumba mwamko wa Kiislamu na
kuharibu utayarifu wa kiroho uliojitokeza katika dunia ya Kiislamu, na kwa mara nyingine
kuyatumbukiza kwa muda mrefu mataifa ya Waislamu katika mkwamo, hali ya kutengwa na
mporomoko na hatimaye kusahaulisha kabisa masuala muhimu ya Waislamu kama kadhia ya
kuikomboa Palestina na mataifa mengine ya Waislamu kutoka kwenye makucha ya Marekani na
Wazayuni.
Tiba mujarabu na ya kimsingi inaweza kufupishwa katika sentensi mbili muhimu ambazo zote ni
katika masomo muhimu ya ibada ya Hija:
Kwanza: Umoja na udugu wa Waislamu chini ya bendera ya tauhidi.
Pili: Kumjua adui na kukabiliana na njama na mbinu zake.
Somo kubwa la ibada ya Hija ni kuimarisha udugu na mshikamano. Hapa, katika ibada ya Hija,
inazuiwa pia kufanya ubishani na malumbano. Vazi la aina moja, amali za aina moja, harakati za
aina moja na mwenendo wa upole hapa katika Hija vina maana ya usawa na udugu wa watu wote
wanaoamini tauhidi. Hili ni jibu la wazi la Uislamu kwa kila fikra, itikadi na wito unaowaondoa
katika Uislamu baadhi ya Waislamu na watu wanaoamini al Kaaba na Tauhidi. Watu wenye
fikra za kuwakufurisha Waislamu ambao wamekuwa wanasesere wa siasa za Wazayuni mahaini
na waungaji mkono wao wa Kimagharibi ambao wanafanya jinai za kutisha na kumwaga damu
za Waislamu wasio na hatia, na wale wanaojidai kushikamana na dini na kuvaa mavazi ya
wanazuoni wa dini wanaochochea moto wa hitilafu kati ya Shia na Suni na wengineo mfano
wao, wanapaswa kuelewa kwamba ibada ya Hija inabatilisha madai yao.
Mimi, kama walivyo maulamaa wengi wa Kiislamu na wale wanaoumizwa na masuala ya Umma
wa Kiislamu, ninatangaza tena kwamba, kila neno au amali inayochochea moto wa hitilafu kati
ya Waislamu, kuvunjiwa heshima matukufu ya mojawapo ya makundi ya Waislamu au
kukufurisha moja kati ya madhehebu za Kiislamu ni kuhudumia kambi ya ukafiri na shirki na
kusaliti Uislamu; na amali hiyo ni haramu.
Kumtambua adui na mbinu anazotumia ndiyo nguzo ya pili. Kwanza kabisa hatupasi kughafilika
na kumsahau adui mwenye kinyongo, na marasimu ya kumpiga mawe mara kadhaa shetani
katika ibada ya Hija ni nembo ya kukumbuka suala hilo daima katika fikra na akili zetu. Pili ni
kwamba hatupasi kufanya makosa katika kumtambua adui yetu asili ambaye hii leo ni kambi ya
ubeberu wa kimataifa na kanali ya watenda jinai ya Kizayuni. Tatu ni kuwa, tunalazimika
kuainisha vyema mbinu za adui huyo mkaidi ambazo ni kuzusha hitilafu kati ya Waislamu,
kueneza ufisadi wa kisiasa na kimaadili, kutoa vitisho na vivutio kwa shakhsia na watu
mashuhuri, kuweka mashinikizo ya kiuchumi dhidi ya mataifa mbalimbali na kuzusha shaka
katika imani na itikadi za Kiislamu na vilevile kuwatambua vibaraka na vikaragosi wao
wanaowafanyia kazi kwa kujua au bila ya kujua.
Madola ya kibeberu yakiongozwa na Marekani yanaficha sura zao halisi kwa kutumia msaada
wa zana za kisasa za vyombo vya habari na kutumia hila na ujanja mbele ya fikra za mataifa
mbalimbali kwa madai ya kutetea haki za binadamu na demokrasia. Madola haya yanadai
kutetea haki za mataifa ilhali mataifa ya Waislamu kila siku yanaona kwa macho na kuhisi kwa
nyoyo moto wa fitina zao. Tunapotazama taifa linalodhulumiwa la Palestina ambalo kwa miongo
kadhaa sasa linaendelea kujeruhiwa kwa jinai za utawala wa Kizayuni wa Israel na waungaji
mkono wake, au katika nchi za Afghanistan, Pakistan na Iraq ambako ugaidi uliotengenezwa na
siasa za ubeberu na vibaraka wao umeyafanya machungu kama shubiri maisha ya mataifa hayo,
3. au nchini Syria ambayo inashambuliwa na chuki za mabeberu wa kimataifa na vikaragosi wao
wa kieneo na imetumbukizwa katika vita vya umwagaji damu vya ndani kwa dhambi ya kuunga
mkono harakati ya mapambano dhidi ya Wazayuni, au Bahrain au Myanmar ambako katika kila
mojawapo ya nchi hizo Waislamu wanaosumbuliwa na mashaka mbalimbali wamesahaulika na
maadui zao wanaungwa mkono, au mataifa mengine ambayo yanatishiwa mara kwa mara na
Marekani na waitifaki wake kushambuliwa kijeshi au kuwekewa vikwazo vya kiuchumi au
kukabiliwa na uharibu wa kiusalama, yote hayo yanaweza kuonesha vyema sura halisi ya vinara
hawa wa mfumo wa ubeberu kwa walimwengu wote.
Shakhsia wa kisiasa, kiutamaduni na kidini katika maeneo yote ya ulimwengu wa Kiislamu
wanalazimika kufichua uhakika huu. Huu ni wajibu wetu sote wa kidini na kiakhlaki. Nchi za
kaskazini mwa Afrika ambazo kwa masikitiko makubwa zimekumbwa na hitilafu kubwa za
ndani, zinalazimika kuliko nchi nyingine, kutilia maanani wajibu huu adhimu, yaani kumtambua
adui, mbinu na njama zake. Kuendelea hitilafu kati ya mirengo mbalimbali ya kitaifa na
kughafilika na hatari ya vita vya wenyewe kwa wenyewe katika nchi hizo ni hatari kubwa
ambayo hasara zake kwa Umma wa Kiislamu haziwezi kufidika haraka.
Hatuna shaka kwamba mataifa yaliyosimama kidete katika eneo hilo linaloonesha kielelezo cha
Mwamko wa Kiislamu, kwa idhini yake Mwenyezi Mungu, hayataruhusu mshale wa saa urejee
nyuma na kurejesha kipindi cha watawala waovu, vibaraka na madikteta; hata hivyo ni wazi
kuwa kughafilika na nafasi ya madola ya kibeberu katika kuzusha fitina na kuingilia mambo yao
ya ndani vitatatiza kazi zao na kuchelewesha kwa miaka mingi kipindi cha izza, usalama na hali
bora ya kimaisha. Tuna imani kubwa na uwezo wa mataifa na nguvu iliyowekwa na Mwenyezi
Mungu Mwenye hikima katika azma, imani na busuri ya watu na tumeiona na kuijaribu nguvu
hiyo kwa macho yetu katika kipindi cha zaidi ya miongo mitatu katika Jamhuri ya Kiislamu ya
Iran. Hima yetu ni kuyalingania mataifa ya Waislamu tajiriba hii ya ndugu zao katika nchi hii
yenye fahari na isiyochoka.
Namuomba Mwenyezi Mungu Mtukufu arekebishe hali za Waislamu na kuwaepusha na vitimbi
vya adui. Vilevile namuomba Mwenyezi Mungu atakabali Hija na kuwapa uzima wa mwili na
roho na tunu kubwa ya kimaanawi ninyi nyote Mahujaji wa Nyumba ya Mwenyezi Mungu.
Wassalaamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakaatuh.
Sayyid Ali Khamenei
5 Dhulhija 1434 Hijria
19 / Mehr/ 1392 Hijria Shamsia
11/ Oktoba/ 2013 Miladia.