UTANGULIZI “Mtazamo Wako Ni Upi?” ni swali mahsusi kwa kila mwanajamii mpenda maendeleo; ukizingatia kuwa “Mtazamo Wako Ni Maisha Yako”. Nasema hivyo nikimaanisha kuwa, jinsi tunavyojichukulia na kujiona tukijilinganisha na uhalisia wa maisha na wa watu wengine ni taswira tosha ya maisha yetu. Hivyo, mtazamo wetu wa maisha huchangia kwa kiasi kikubwa katika mafanikio au kushindwa maishani kutegemeana na aina ya mtazamo tulionao. Katika kitabu hiki mwandishi makini anakuleta moja kwa moja na kukuonyesha mbinu stahiki- hatua kwa hatua ili kuuweka mtazamo wa maisha yako katika hali iliyo thabiti, yenye kuleta mafanikio na furaha maishani. Nyanja mbali mbali zenye kuhitaji mabadiliko au maboresho ya kimtazamo kama biashara, elimu, ajira, maisha na malezi ya familia yenye maadili na mazingira zimeainishwa kwa mifano fasaha, pia katika hatua na mbinu stahiki ili kukuwezesha msomaji kufuatilia mbinu moja hadi nyingine kujiletea mabadiliko chanya. Natumaini kila mtu anapenda kufanikiwa kimaisha, hivyo ni vyema kuzijua mbinu tajwa ndani ya kitabu hiki zitakazokupeleka kwenye mtazamo wa mafanikio maishani. Kitabu hiki si cha kukikosa, kinampa msomaji uhuru wa kuchagua kusoma SURA aipendaye kwa wakati husika. Ni kitabu rafiki kwa kila mpenda maendeleo na mabadiliko yenye mafanikio maishani. Ahsante na Karibu.